MAKAMU Mkuu wa Chuo Kikuu Huria Prof. Tolly Mbwete amewataka wanafunzi nchini kuendelea na elimu ya vyuo vikuu hadi mwisho ili kupunguza pengo kubwa la wasomi nchini.
Profesa Mbwete alisema Tanzania ya sasa inakabiliwa na upungufu mkubwa wa wasomi kuliko wajinga na kwamba kinachotakiwa ni kwa vijana kujifunga vibwebwe katika elimu ya vyuo vikuu.
Alisema kwa mujibu wa utafiti uliofanywa katika mikoa mbalimbali hapa nchini vijiji vingi havina wataalamu wasomi wa elimu mbalimbali hususan ya ufundi.
Profesa Mbwete alisema hayo alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa Zoom Poltechinic College kwa niaba ya Waziri wa Mali Asili na Utalii ambapo aliwataka wanachuo hao kusoma kwa malengo ya elimu ya juu zaidi na si kutaka kuishia katika ngazi ya stashahada.
"Katika suala la elimu taifa hili bado tuko nyuma kwa sababu nchi zilizoendelea, kiwango chao cha elimu ni asilimia 40 wakati hapa ni asilimia 10,"alisema Prof. Mbwete.
Alisema utafiti umebaini shida zilizoko vijijini jinsi watu wanavyopata shida ya kupata wataalamu wa kufanya kazi, hali inayowalazimu kutumia gharama kuwatoa mijini kwenda kufanya kazi au kutengeneza kitu fulani.
Alisema jitihada za kupata wasomi wengi zitafanikiwa ikiwa watu wengi wataendelea kuwekeza katika elimu na kwamba lengo liwe kupata wasomi wa taaluma mbalimbali.
Akizungumzia chuo hicho, Profesa huyo alimpongeza Mkurugenzi wa chuo hicho, Gaudios Shija kwa mafanikio aliyoyapata kwa kipindi kifupi tangu aanzishe chuo hicho mwaka 2000.
Hata hivyo aliwataka wanafunzi kutumia nafasi walizopata kusoma kwa bidii ili waweze kuendelea na vyuo vikuu vingine.
source: mwananchi.

Rais Omar Al- Bashir alishtakiwa kwa madai ya ukatili dhidi ya raia katika eneo la Darfur, magharibi mwa Sudan mwezi wa tatu.
Lakini wajumbe katika mkutano wa AU uliofanyika nchini Libya walikubaliana kuhusu azimio linalosema hawatatoa ushirikiano katika kukamatwa kwa Rais Bashir.
Wadadisi wanasema hatua hiyo ina maana kwamba rais Bashir anaweza kusafiri popote barani Afrika ya hofu ya kukamatwa.
Serikali ya Sudan imekuwa ikipigana na waasi katika jimbo la Darfur tangu mwaka 2003.
Mahakama ya ICC inamshtaki Rais Bashir kwa makosa mawili ya uhalifu wa kivita ; kuagiza kushambuliwa kwa raia na uporaji , pamoja na mashtaka mengine matano ya uhalifu dhidi ya binadamu , mkiwemo mauaji , ubakaji na utesaji , yote hayo yakihusishwa na mzozo huo.
Ameyakanusha mashtaka hayo yote , akisema serikali inao wajibu wa kupambana na makundi ya waasi.
Kwenye taarifa , AU imeeleza kwamba ombi lake la kuitaka mahakama ya ICC iliyoko mjini The Hague isimamishe kwa muda hoja hiyo ya kukamatwa kwa Rais Bashir limepuuzwa.
Taarifa jiyo inasema : '' Umoja wa Afrika hautatoa ushirikiano kuhusiana na hoja ya kukamatwa au kujisalimisha kwa Rais wa Sudan Omar Al- Bashir kwa mahakama ya ICC.''
Mwandishi wa BBC anasema ingawa taarifa hiyo imeungwa mkono na viongozi wengi wa Afrika , bado kuna nchi kadhaa , zikiwemo Chad na Benin ambazo zinaonekana kutoridhishwa na kauli hiyo.
Pia kumekuwa na maswali kuhusu taarifa hiyo, kwa sababu haijazitaka nchi 30 zilizotia sahihi ya kuundwa kwa mahakama ya ICC kusitisha uhusiano na mahakama hiyo.
Uamuzi huo ulifanyika katika siku ambapo Kenya imekubali kuendelea kushirikiana na mahakama hiyo ya ICC , kuwashtaki wale wanaotuhumiwa kwa kuchochea ghasia zilizofuatia uchaguzi wa mwezi Disemba mwaka 2007.
Watu wa watatu wamefariki dunia na mmoja kujeruhiwa vibaya katika ajali za barabarani zilizotokea katika maeneo tofauti Jijini Dar es Salaam jana.
Akizungumzia kuhusiana na tukio la kwanza, Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Mark Kalunguyeye amesema lilitokea saa 9:30 usiku wa kuamkia jana katika barabara ya Haile Selasi, maeneo ya Oysterbay na kulihusisha gari aina saloon lenye namba za usajili T 555 AJV.
Amewataja waliofariki kuwa ni dereva wa gari hilo na mkazi wa Upanga, Jalvad Gama , 32 na abiria mmoja mkazi wa Masaki aliyetambuliwa kwa jina la Sailen Gilan, 50. Amesema katika ajali hiyo mtu mmoja aitwaye Gurminber Jandu , 30 alijeruhiwa.
Kamanda Kalunguyeye amesema ajali hiyo ilitokea baada ya dereva aliyekuwa akitokea Masaki kwenda barabara ya Ali Hassan Mwinyi, kushindwa kulimudu gari na kugonga mti.
Amesema miili ya watu hao imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Aghakhan.
Amesema majeruhi huyo ambaye ni mkazi wa Masaki na fundi magari, anaendelea na matibabu katika hospitali ya Aghakhan.
Katika tukio la pili, Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Ilala, Faustine Shilogile amesema mwenda kwa miguu mmoja amefariki dunia baada ya kugongwa na gari lisilofahamika.
Amesema ajali hiyo ilitokea jana saa 12:15 asubuhi katika eneo la Tazara wakati mwenda kwa mguu huyo ambaye ni mwanamke anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 30-35, alipokuwa akivuka barabara ya Nyerere.
Amesema gari wala dereva aliyemgonga hakufahamika na kwamba mwili wa marehemu umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.


Mazishi ya Mfalme wa Pop Duniani Michael Jackson yamegeuka kuwa 'dili' la aina yake baada ya watu kibao kugombea nafasi ya kuhudhuria shughuli hiyo.
Taarifa zinaeleza kuwa hadi sasa, zaidi ya watu 500,000 wamejisajili kwa ajili ya kucheza bahati nasibu ya kuwania tiketi kiduchu, zinazotajwa kuwa ni 17,500 pekee ili kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa Michael Jackson.
Uwanja wa mpira wa kikapu wa Staples Center Jijini Los Angeles ndio utakaotumika Jumanne ijayo kwa shughuli za kumuaga mwanamuziki huyo aliyefariki ghafla Alhamisi iliyopita.
Hata hivyo, wakati watu kibao wakiwania kushiriki mazishi ya mfalme huyo wa pop duniani, familia yake bado haijaeleza ni siku gani hasa atazikwa.
Sakataka hilo lilitokea Jumatano wiki hii katika kijiji cha DDC mji mdogo wa Mbalizi Wilaya ya Mbeya Vijijini baada ya kijana huyo kufika nyumbani kwao na kukuta watu wameweka tanga.
Kitendo hicho kilizua tafrani na waombolezaji hao kutimua mbio wakidhani muzimu umeibuka.
Majira baada ya kusikia taarifa hizo, lilifuatilia hadi kijijini hapo, umbali wa kilomita 15 kutoka Mbeya mjini kujionea kulikoni.
Akithibitisha kutokea tukio hilo Mwenyekiti wa kijiji hicho, Bw. Joines Mwalusanya, alisema kifo hicho kilitokea June 27 mwaka.
Alisema walipelekewa taarifa ofisi ya kijiji kuwa kuna kijana amepigwa na wananchi wenye hasira na amefia Hospitali ya Rufaa Mbeya.
Alisema waliambatana na ndugu wa kijana huyo kwenda kutambua maiti Hospitali ya Rufaa Mbeya na kubaini kuwa marehemu huyo alikuwa ni Frank.
Hata hivyo, alisema babu wa kijana huyo Mzee Joyasi Mboma alikataa kuwa kijana huyo si mjukuu wake Frank kutokana na kuonesha tofauti za sehemu fulani mwilini japo alionekana kufanana naye kwa sehemu kubwa.
Baadaye alisema bibi wa kijana huyo na kinyozi aliyekuwa amemnyoa, walithibitisha kuwa ndiye na kuamua kuchukua kibali Polisi na kuzika Juni 29 jioni na kuendelea na matanga nyumbani kwa Mzee Mboma eneo hilo la DDC.
Naye Mzee Mboma ambaye amemlea kijana huyo akitoa maelezo yake kwa waandishi wa habari alisema mjukuu wake aliondoka wiki moja kwenda Tunduma kutafuta maisha hadi aliposikia habari kwamba kuna maiti inayofanana naye na baada ya utata alikubali kuzika mwili huo.
Alisema kuwa alishangaa Jumatano kufuatwa na watu na kuambiwa mjukuu wake amefika eneo jirani na kwake na anaogopa kuingia ndani baada ya kuambiwa alikuwa amekufa na kuzikwa na watu wamekusanyika kwa ajili ya msiba wake.
"Nilikwenda ingawa ilikuwa usiku wa manane, nilishangaa kumkuta Frank akiwa hai. Nilimchukua na kuingia naye ndani, baada
ya kumhoji tuligundua kuwa ni mjukuu wangu na tuliyemzika siye,"alisema Mzee Mboma.
Alisema kuwa kesho yake walikwenda Polisi kutoa taarifa na kuambia waende na Frank kwa ajili ya mahojiano zaidi ili kuondoa utata.
Akiwa Polisi Frank alieleza kuwa baada ya kwenda Tunduma kutafuta maisha alijisikia roho ikiuma na kuamua kurudi kwao mara moja ndipo alipokuta msiba wake bandia.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Bw.Advocate Nyombi hakupatikana kuzungumzia sakata hilo lakini ofisa mmoja katika ofisi yake ambaye hakutaka kutajwa jina lake kwa kuwa si msemaji, alisema wamepata taarifa za tukio hilo na walikuwa wanasubiri maelezo kamili kutoka kwa maafisa wa Jeshi hilo waliokuwa wakifuatilia tukio hilo.





