Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

AL-SHABAAB YATISHIA KUSHAMBULIA MIKOA YA KASKAZINI MASHARIKI YA TANZANIA



KUNDI la kigaidi nchini Somalia lenye uhusiano na al Qaeda, la al Shabaab limetishia kufanya mashambulizi Tanga na Kilimanjaro na tayari vyombo vya usalama mkoani Kilimanjaro, vimetoa hadhari katika maeneo ya viwanda vinavyoweza kushambuliwa.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Absalom Mwakyoma, alithibitisha kuwapo kwa tishio hilo lakini alikataa kuzungumzia zaidi kwa madai ni la kiusalama zaidi.

“Hilo jambo lipo lakini sitalizungumzia, kwani ni mambo ya kiusalama zaidi…wewe nani amekupa taarifa hizo, muulize aliyekwambia akufafanulie,” alisema.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Ofisa Mtendaji Utawala wa Kiwanda cha Sukari cha TPC, Jaffary Ali, wamepewa taarifa za kuchukua hadhari juu ya kuwapo kwa tishio la shambulio kiwandani hapo.

Alisema taarifa hizo zimetolewa na Kamanda Mwakyoma baada ya kupata taarifa mbalimbali za kiusalama zilizopatikana juu ya kuwapo kwa tukio hilo.

“Ni kweli tumepata taarifa za kuwapo kwa shambulio la kikundi cha al Shabaab lakini haijataja moja kwa moja kwamba sisi ndio tunashambuliwa ila tumetakiwa kujihadhari na watu, magari na hata pikipiki, tusizozifahamu,” alisema.

Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda Mwakyoma, huenda kikundi hicho kikatekeleza mashambulizi yao kwa kutumia pikipiki, jambo ambalo linasababisha kutilia shaka vyombo vyote vya usafiri vinavyopita kiwandani hapo.

Alisema kutokana na taarifa hizo, tayari kiwanda kimetoa hadhari kwa wafanyakazi wake, viongozi wa vijiji vinavyozunguka kiwanda pamoja na familia za wafanyakazi kuwa makini
dhidi ya watu wasiowafahamu.

“Kwa mujibu wa taarifa ya Kamanda, kwa Tanga kimetajwa kiwanda cha saruji, lakini huku kwetu tumehadharishwa katika maeneo haya ya viwanda, kwani ndiyo lengo lao, tumewataka wafanyakazi wasiwe na hofu, lakini pia tunaendelea na kazi,” alisema.

Alisema menejimenti imeimarisha ulinzi katika eneo la kiwanda, lakini pia imeagiza mbwa maalumu wa kutambua mabomu kutoka Arusha ili kusaidia ukaguzi wa maeneo yote.

Alisema wafanyakazi wa mashambani wamepewa taarifa kuhusu ubebaji miwa, kwani huenda
wakabeba bomu na kuliingiza kiwandani, iwapo kikundi hicho kitatega kupitia mashamba.

"Hawa mbwa tulioagiza watafanya doria maeneo yote ya kiwanda na mashamba kutokana na
hofu kwamba wakitumia mashamba ni rahisi kuyabaini," alisema.

Kwa upande wao, baadhi ya wafanyakazi wa kiwanda cha TPC, waliojitambulisha kwa jina moja la Mziray na Juma, walisema tishio hilo limeleta hofu, kwani athari za mashambulizi ya kikundi hicho ni makubwa.

Alisema wameshuhudia mara kadhaa kupitia vyombo vya habari, katika nchi za Kenya na Uganda, jinsi ambavyo vimeshambuliwa na kikundi hicho na kusababisha vifo vya mamia ya wananchi wasio na hatia.

"Hili tishio limetulazimu kuhamisha baadhi ya wanafamilia wetu, tumewataka waende mjini
Moshi kuishi na ndugu," alisema.

Akizungumzia taarifa hizo, mkazi wa kijiji cha Langasani wilayani Moshi vijijini, Abdul Sultan, alisema ni vyema Serikali ikaimarisha usalama katika mipaka ili kudhibiti kikundi hicho.

Alisema pamoja na suala la mipaka ya nchi, lakini pia zipo sababu za msingi kwa wananchi kupewa elimu ya utambuzi wa watu wenye nia ovu ili iwasaidie kukabiliana na watu hao.

Kikundi cha al Shabaab kimekuwa kikifanya vitendo vya ugaidi ndani ya Somalia, Uganda na Kenya hata kulazimu majeshi ya Kenya kuingia nchini Somalia kukabiliana nacho.
[ Read More ]