Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

Watoto 4750 Wanaishi Mazingira Magumu Wete



WATOTO 4750 kutoka shehia 22 za wilaya ya Wete wanaishi katika mazingira magumu mno, utafiti uliofanywa na kitengo cha hifadhi ya mtoto Pemba, umebainisha.

Afisa kutoka kitengo cha hifadhi ya mtoto Pemba, Raya Said aliliambia gazeti hili katika mahojiano maalum kwamba, watoto hao walibainika katika kaya zote zilizo ndani ya wilaya hiyo.


Alisema hao ni wale wanaoishi katika mazingira magumu mno, ambao hawana msaada wala usaidizi wowote, ambapo miongoni mwao wapo pia wanafunzi wa kike.

Shehia zilizoandikisha rekodi ya juu ni Kojani ambapo watoto 186 wakiwemo wanawake 83 wanaishi katika mazingira ya kusikitisha.

Shehia nyengine ni Kigongoni yenye watoto 386 wakiwemo wanawake 201, Mtambwe kaskazini watoto 281 wakiwemo wanaume 117, Pembeni watoto 121, Gando (126), Junguni (100) na Kisiwani watoto 115.

Raya alisema tatizo kubwa linalowakabili watoto hawa ni huduma muhimu za kijamii ikiwemo chakula cha uhakika, mavazi, malazi na matunzo kutoka kwa familia zao, hali iliyowafanya wengi kuishi katika maisha ya kukata tamaa.

Aidha alisema baadhi ya watoto hawana sare za skuli na wale walionazo zimechakaa mno.

Hali hiyo imewafanya watoto wengi kukatisha masomo na kujishughulisha na ajira mbadala ambazo ni hatari kwa afya zao.

Afisa huyo alisema baadhi ya familia zimekuwa zikiwatumia watoto hao kama mtaji; kwa kwenda kufanya kazi ili waendeshe familia zao ikiwemo kupara samaki.

Aliziomba asasi za kiraia za kitaifa na kimataifa kushirikiana na kitengo chake kusaidia kumkomboa mtoto na kumuweka katika mazingira bora kielimu na kiafya.
[ Read More ]

Wanafunzi 19 Waozeshwa Waume, Wapewa Mimba Chake



WANAFUNZI 19 walipewa mimba na kuozeshwa waume katika skuli 9 za wilaya ya Chake kuanzia mwaka 2008 hadi mwaka uliopita, wakiwemo wanafunzi wawili wa darasa la tano na saba kutoka skuli za Vitongoji na Pujini ambao wote walipewa mimba.

Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba, wanafunzi sita walipewa mimba au kuolewa katika skuli ya Ndagoni mwaka 2008 pekee.


Aidha wanafunzi wengine watatu wa kidato cha tatu kutoka skuli ya Kilindi na mmoja wa kidato cha kwanza kutoka skuli ya Pujini walikutwa na masaibu kama hayo mwaka 2009.

Hali kama hiyo ilitokea mwaka 2010 katika skuli za Vikunguni, Chanjamjawiri, Shamiani, Uwandani na Birikau, ambapo jumla ya wanafunzi watano wa kuanzia darasa la saba hadi kidato cha pili walipewa ujauzito au kuozeshwa waume.

Kwa mwaka uliopita jumla ya kesi nne zimeripotiwa katika skuli za Vikunguni, Pujini, Shamiani na Vitongoji ambapo wanafunzi watatu wa darasa la tano, saba na kidato cha pili walipewa ujauzito na mmoja wa kidato cha tatu kupewa mume.

Aidha kesi 113 zinazohusisha ubakaji, mimba, kuozeshwa waume na ukatili mwengine wa kijinsia ziliripotiwa katika wizara ya Ustawi wa Jamii Pemba katika kipindi cha Julai 2010 hadi Juni 2011.

Mkoa wa Kusini Pemba uliandikisha kesi 67 zikiwemo sita za ubakaji na 32 za utelekezaji watoto.

Afisa Mipango Wizara ya Ustawi wa Jamii, Maendeleo ya Wanawake na Watoto Pemba, Salama Mbarouk Khatib , alisema tatizo hilo zaidi limechangiwa na ushawishi wa kundi rika.

Alisema baadhi ya wanafunzi wa kike wamekuwa wakiwashawishi wenzao kuanzisha uhusiano wa kimapenzi ili waweze kufaidika na fursa walizonazo wao.

Alisema changamoto nyengine ni kukosekana huduma muhimu katika skuli zenye dakhalia, ambapo mtoto wa kike hulazimika kutafuta chakula kwa gharama zake, akiwa mbali ya wazazi wake, ambao hata hivyo wengi hushindwa kuwakamilishia mahitaji kwa sababu ya umaskini.

Salama alisema baadhi ya wazazi wamekuwa ving'ang'anizi kwa kulazimisha watoto wao kuolewa hata kama wao hawako tayari.

"Tumeshuhudia wazazi wakimsusa mtoto wao na kufikia hatua ya kumfichia sare zake na mabuku kuyachoma moto kwa sababu tu amekataa kuolewa," alisema.

Mkuu wa wilaya ya Chake Chake, Mwanajuma Majid Abdalla kwa upande wake, alisema katika miaka ya nyuma tatizo hilo pia lilikuwa linachangiwa na walimu ambao walikuwa wakiwadhalilisha wanafunzi wa kike kingono.

Hata hivyo, alisema wilaya kwa kushirikiana na taasisi nyengine wamekabiliana na walimu hao kwa kuwakumbusha kuzingatia maadili yao.

Alisema wilaya kwa ushirikiano na maafisa wa elimu na kutoka wizara ya jinsia wamefanikiwa kuzivunja ndoa nyingi, ambazo ziliwahusisha wanafunzi wa kike.

Afisa Mipango, Sera na Utafiti kutoka wizara ya Elimu Pemba, Khamis Ali alisema tatizo la mimba, ndoa za kushurutishwa zimekuwa zikipungua kutokana na mwamko walionao wanafunzi pamoja na wazee wengi.

Aidha alisema kukosekana huduma za dakhalia pia inaweza kuwa moja ya vyanzo vya matukio hayo, ambayo yanaathiri maendeleo ya elimu ya mtoto wa kike.
[ Read More ]