Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

JK Ziarani Uturuki






Rais wa Uturuki Abdullah Gul na mkewe wakiwakaribisha ikulu ya jıjını Ankara JK Mama Salma leo asubuhi

JK na mwenyeji wake Raıs wa Uturuki Abdukkah Gul wakıkagua gwaride la heshima muda mfupi baada ya Rais Kıkwete kuwasili katika ikulu ya nchı hıyo iliyopo jijini Ankara leo asubuhi.


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo 18 Feb, 10 anaanza ziara ya siku tatu nchini Uturuki kwa makaribisho rasmi ambapo Rais wa Uturuki Mheshimiwa Abdullah Gul atamkaribisha Rais Kikwete katika kasri ya nchi hiyo.

Mara baada ya makaribisho hayo, viongozi hao wawili watafanya mazungumzo rasmi ya kiserikali na kushuhudia utiaji saini kwa mikataba mitano kati ya nchi mbili hizi shughuli ambazo zitafanywa na mawaziri.


Mchana wa leo, (18.2.10) Rais na ujumbe wake utakutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Uturuki, Mheshimiwa Recep Tayyid Erdogan kabla ya kukutana na kufanya mazungumzo na spika wa Bunge la Uturuki Mheshimiwa Mehmet Ali Sahin.

Rais Kikwete pia atakutana na kufanya mazungumzo na Umoja wa Wafanyabiashara wa Uturuki na baadaye kukutana na mabalozi wa Nchi za Afrika waliopo Uturuki na baadaye jioni hii Rais Kiwete na ujumbe wake watahudhuria dhifa ya kitaifa iliyoandaliwa kwa heshima yake na mwenyeji wake.



[ Read More ]

Ajiua baada ya kumchinja mkewe kwa wivu

MKAZI wa Kitefu wilayani Arumeru mkoani hapa, George Lukas (27), anatuhumiwa kumuua mkewe kwa kumchinja na kisu na kisha kuacha ujumbe mzito, kabla naye kujiua kwa sumu kutokana na wivu wa mapenzi.

Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Basilio Matei alisema tukio la kuuawa kwa mke huyo, Asumin Hussein (36), limetokea juzi saa 12 jioni katika Kitongoji cha Kitefu, Maroroni wilayani Arumeru.

Akielezea chanzo cha tukio hilo, Kamanda Matei alisema wanandoa hao wamekuwa na ugomvi wa mara kwa mara, huku mume akimtuhumu mkewe kuwa sio mwaminifu kwani amekuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamume mwingine, na kwamba amewahi kutoa ujauzito wake ili aolewe na mwanamume mwingine.

Alisema siku ya tukio, mwanamume huyo alifika nyumbani na kuanza kudai ujauzito wake kutokana na majibizano, kulitokea ugomvi wa kutoelewana, na kusababisha mume kuchukua kisu na kumchinja mkewe, na kusababisha kifo cha mwanamke huyo.

Baada ya tukio hilo, Kamanda alisema Lukas alichukua karatasi na kuandika ujumbe kabla ya kujiua kwa sumu, ambayo haikufahamika.

Polisi baada ya kupata taarifa, walifika eneo la tukio na kukuta karatasi yenye ujumbe uliosomeka kuwa “nimeamua kumuua mke wangu kwa sababu ametoa mimba yangu na ana uhusiano na mwanamume mwingine.’’

Katika tukio jingine, Lembrisi Taiko (25), mkazi wa Sanawari Moivo katika Manispaa ya Arusha, ameuawa kwa kukatwakatwa na panga na wananchi baada ya kujeruhi kwa panga.

Kamanda Matei alisema tukio hilo limetokea juzi saa 4:30 usiku baada ya Taiko kukutwa akimshambulia kwa panga, Saimoni Lizer (45) na kumjeruhi vibaya kwa sababu ambazo hazikufahamika.

Miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru kwa uchunguzi zaidi.
[ Read More ]

Mtoto aliyenusurika mauaji Musoma asimulia alivyookoka

MTOTO wa miaka minne aliyenusurika katika mauaji ya watu 17 wa familia tatu za ukoo mmoja katika eneo la Buhare, nje ya Manispaa ya Musoma, mkoani Mare, ameeleza namna alivyojiokoa dhidi ya wauaji kwa kuingia uvunguni.

Kituo cha Redio Clouds jana kilirusha sauti ya mtoto huyo (jina lake limehifadhiwa) akijieleza kwamba alifanikiwa kuingia uvunguni mwa kitanda mara baada ya wahalifu hao kuanza kuwakata kwa mapanga ndugu zake.

Mtoto huyo ambaye kwa mujibu wa mwandishi wa kituo hicho alionekana kisaikolojia kuathirika kutokana na tukio hilo, alisikika akisema hakuweza kuwatambua wavamizi kutokana na jinsi walivyojifunika makoti meusi.

Akielezea walivyoonekana, mtoto huyo ambaye kwa mujibu wa mahojiano redioni alikuwa amefuatana na watu wazima, akiwamo kiongozi wa ukoo, alidai kuwa aliwaona watu wanne waliokuwa na makoti meusi na viatu alivyovitaja kwamba vinafanana na vya kuchezea mpira.

Alisema aliwasikia wakiwataka wanafamilia hao kutoa fedha na kuwaambia wasipotoa, watawaua.

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Enos Mfuru, wakati wa maziko ya miili ya watu waliouawa kwenye tukio hilo ambalo kati ya marehemu 17, kati yao, 11 ni watoto wenye umri wa kati ya miezi 11 na miaka 13 wakiwamo wazazi wake, aliahidi kwamba Serikali itamhudumia mtoto huyo.

Mfuru alisema mtoto huyo atasomeshwa na Serikali. Naye Mbunge wa Musoma Vijijini, Vedastus Mathayo (CCM), aliahidi kumsaidia.

Mfuru alisema Serikali itahakikisha inagharimia matibabu kwa majeruhi wa tukio hilo waliolazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Mara mjini Musoma. Maiti hao 17 walizikwa juzi katika tukio lililohudhuriwa na mamia ya watu.

Taarifa zinasema mauaji hayo yalifanyika kutokana na kinachosadikiwa kuwa ni kulipiza kisasi. Polisi katika taarifa yake ya juzi, ilisema watu watano walikuwa wamekamatwa wakihojiwa juu ya tukio hilo.

Miili 16 ilizikwa katika kijiji cha Mgaranjabo nje kidogo ya Musoma na aliyekuwa mwanafunzi wa sekondari ya Mkirira, Joseph Sofareti, alisafirishwa kwenda kijijini kwao Kome, Musoma Vijijini baada ya heshima za mwisho kutolewa.
[ Read More ]

Aanguka toka ghorofa ya tisa

FUNDI ujenzi aliyefahamika kwa jina moja la Ally, amekufa baada ya kuanguka kutoka ghorofa ya tisa wakasti akiwa katika shughuli za ujenzi katika ghorofa hiyo.

Fundi huyo alikuwa katika ya nyumba ya Shubas Patel iliyokuwa na ghorofa 12 na alianguka wakati akiwa kazini.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile, amesema ajali hiyo ilitokea jana, saa 10 jioni, Mtaa wa Sewa na Zanaki Ilala jijini Dar es Salaam.

Alisema fundi huyo, akiwa na wenzake wakiendelea na kazi kwenye ghorofa ya tisa, ghafla alidondoka hadi ghorofa ya tatu ambapo alinasa kwenye kizuizi cha mabati.

Alisema alipata majeraha kwenye paji la uso pamoja na kuvunjika mkono wake wa kushoto.

Hata hivyo wenzake walimkimbiza Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu na alikufa muda mfupi baada ya kufikishwa hospitalini hapo.


SOURCE;NIFAHAMISHE.COM
[ Read More ]

Mstaafu JWTZ mbaroni kwa tuhuma za kumuua mkewe

ASKARI mstaafu wa Jeshi la la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Matiko Ng'eng'e (55) anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumuua mkewe kwa kisu.

Ng'eng'e ambaye alikuwa sanjenti wa jeshi hilo anadaiwa kufanya hivyo saa 11:00 alfajiri ya jana nyumbani kwake Ukonga Mazizini, jijini Dar es Salaam.

Habari ambazo Mwananchi imezipata na kuthibitishwa na Polisi zilisema mauaji hayo yalifuatia mgogoro wa shamba ambalo mtuhumiwa alikuwa ashinikiza liuzwe huku mkewe akipinga vikali mpango huo.

Akisimulia mkasa huo nyumbani kwao, mtoto wa mtuhumiwa huyo, Joyce Matiko (22) alidai kuwa baba yake ana wake wawili wa ndoa na kwamba marehemu alikuwa ni mke mdogo.

Kwa mujibu wa Joyce, mke mkubwa wa baba yake anaishi Banana.

Alisema hata hivyo familia hizo zimekuwa katika mgogoro wa muda mrefu kuhusu eneo ambalo mke mdogo na watoto wake wamekuwa wakiishi na kwamba mgogoro huo ulitokana na baba yao kutaka eneo liuzwe ili apate fedha za kusafirisha familia kwenda kijijini.

"Muda mfupi kabla ya mauaji ya mama yetu, baba alituita watoto wote watano pamoja na mama na kutukanya tusithubutu kuuza eneo tunaloishi hata kama itatokea yeye amekufa.

Tulishangazwa sana baba kutuita na kutukanya eti tusithubutu kuuza eneo hilo, wakati yeye ndiye kinara wa kutafuta madalali kwa siri ili afanikishe zoezi hilo,"alisisitiza mtoto huyo.

Alisema mara baada ya kikao hicho, baba yao aliwataka warudi ndani wakalale na kwamba walifanya hivyo.

Mtoto huyo alisema ilipofika saa 9:30 usiku alisikia kelele za mama yao akiomba msaada kwamba anakufa na kuomba asaidiwe jambo lilowashtua mno.

Alisema baada ya kusikia kelele hizo waliamua kutoka na kumkuta mama yao akiwa amelala chini huku damu zikiwa zinamtoka kwa wingi mwilini.

"Tulimkuta mama akiwa amelala chini katika dimbwi la damu, lakini baba hakuwepo alikuwa amejifungia chumbani, tulipiga kelele za kuomba msaada na muda mfupi tu majirani walifika na kutusaidia kumtoa kabla polisi kufika," alisema.

Alisema baada ya polisi kufika walimchukua mtuhumiwa (baba yao) na mama yao ambaye kwa wakati huo alikuwa ameshapoteza maisha.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ilala, Faustine Shilogile, alisema polisi wanamshikilia mtuhumiwa huyo katika Kituo cha Polisi cha Staki Shari, wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.

Kamanda Shilogile alisema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Amana, kwa uchunguzi na kwamba upelelezi ukikamilka mtuhumiwa atafikishwa mahakamani mara moja.

[ Read More ]

GIZA ZANZIBAR LASABABISHA NDEGE YA NAHODHA KUKWAMA KUTUA

Ndege ya Serikali ikiwa imembeba Waziri Kiongozi, Shamsi Vuai Nahodha, imeshindwa kutua katika Uwanja wa Kimataifa wa Zanzibar kutokana na giza baada ya jenereta ya kufua umeme wa dharura kuharibika.

Waziri Kiongozi alikuwa akitokea mkoani Dodoma kuhudhuria kikao cha Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM akiwa amefuatana na Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Zanzibar, Shawana Buheit Hassan ambaye pia ni mjumbe wa NEC.

Taarifa zilizopatikana zimeeleza kwamba ndege hiyo iliondoka juzi saa 12:00 jioni mjini Dodoma na ilitarajia kutua saa 1:00 usiku katika Uwanja wa Kimataifa wa Ndege Zanzibar.

Hata hivyo, kutokana na uwanja huo kuwa gizani, ndege hiyo ilizunguka mara kadhaa katika anga ya Zanzibar na baadaye kwenda kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Meneja wa Mamlaka ya Usalama wa Usafiri wa Anga Zanzibar, Said Sumri, alithibitisha kuwa ndege hiyo ilishindwa kutua Zanzibar ikiwa na wajumbe wa NEC.

Hata hivyo, Sumari hakutaka kuingia kwa undani zaidi juu ya suala hilo kwa madai kwamba si msemaji.

Lakini vyanzo vya habari katika tukio hilo vilieleza kwamba ndege hiyo ililazimika kuzunguka katika anga ya Zanzibar na baadaye kurejea Dar es Salaam na kutua katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

“Tulilazimika kulala Dar es Salaam baada ya ndege yetu kushindwa kutua kutokana na tatizo la giza kufuatia jenereta ya uwanja kuharibika,” chanzo kimoja cha habari kilikaririwa kikisema.

Hata hivyo, abiria wote waliokuwemo katika ndege hiyo baada ya kuwasili jijini Dar es Salaam, walilazimika kujihudumia gharama za hoteli na kulazimika kusafiri Zanzibar siku iliyofuata na kuwasili Zanzibar saa 4:00 asubuhi jana.

Baadhi ya viongozi waliokuwemo ndani ya ndege hiyo ni wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, Salmin Awadh Salmin (Magomeni), Ali Suleiman Ali (Kwahani), Thuwaiba Kisasi (Viti Maalum), Zainab Shomari (NEC), Issa Ahmed Othman (NEC) na wasaidizi kadhaa wa Waziri Kiongozi.

Lakini Mkurugenzi wa Uwanja wa Ndege Zanzibar, Malik Mohammed Hanif, alisema ndege hiyo ilishindwa kutua Zanzibar kwa vile uwanja wa ndege upo katika matengenezo.

Alisema tangu kuanza matengenezo katika uwanja huo, umekuwa ukifungwa kuanzia saa 1:00 usiku ili kuweka mazingira ya utulivu wakati mafundi wakitekeleza majukumu yao.

“Ndege ilishindwa kutua kutokana na matengenezo yanayoendelea katika uwanja huo na sio kweli kama jenereta liliharibika ghafla," alisema Mkurugenzi huyo.

Zanzibar haina huduma za umeme tangu Desemba 10, mwaka jana na kuathiri sekta za kiuchumi na kijamii, baada ya waya unaopokea umeme kutoka Tanzania Bara kulipuka katika kituo cha Fumba Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.

Kutokana na tatizo hilo, taasisi mbalimbali zimekuwa zikitumia umeme wa dharura wa majenereta, ikiwemo Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar ambao hivi sasa upo katika matengenezo makubwa yanayofanywa na Kampuni ya Sogea Satom ya nchini Ufaransa.

Uwanja huo wa ndege unatarajiwa kuongezwa urefu kutoka mita 2,662 hadi 3,022 na mradi huo unatarajiwa kukamilika Agosti, mwaka huu.
[ Read More ]