Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

Wauliwa Kwa Kufunga Ndoa Bila ya Idhini ya Wazazi - Pakistan

Binti mmoja wa nchini Pakistan ambaye alitoroka nyumbani kwao na kwenda kuolewa bila ya idhini ya wazazi wake ameuliwa yeye na mumewe kwa kupigwa risasi na ndugu zake ambao walidai wanasafisha aibu iliyowekwa na binti huyo. Ndugu wa binti huyo wakiwa wamevalia unifomu za polisi walivamia nyumba aliyokimbilia binti huyo baada ya kuolewa kisiri na kuwaua watu wote waliokuwemo ndani ya nyumba hiyo.

Polisi wa Pakistan walisema kwamba kundi kubwa la ndugu wa binti huyo walivamia nyumba ambayo binti huyo na mumewe walikuwa wakikaa kwenye kitongoji cha Charsadda, kilichopo kaskazini magharibi mwa Pakistani.

"Kundi hilo lilimchukua bwana harusi na kumtoa nje ya nyumba hiyo kabla ya kumuua kwa kumpiga risasi, wakati baadhi yao wakiingia ndani na kumuua bi harusi, mama na dada wa bwana harusi" alisema afisa wa polisi wa eneo hilo.

"Waliwapiga kwanza kisha wakawaua kwa kuwapiga risasi" alisema afisa huyo.

"Baba wa bwana harusi naye aliuliwa" alisema afisa mwingine wa polisi alipohojiwa na shirika la habari la AFP.

Bi harusi alikuwa na umri wa miaka 19 wakati bwana harusi alikuwa na umri wa miaka 29.

Polisi walisema kwamba binti huyo wa kitongoji cha jirani alikimbia nyumbani kwao na kwenda kuolewa kwenye kitongoji hicho bila ya ruhusa ya wazazi wake.

"Walikuwa wameoana wiki chache tu zilizopita" alisema mjomba wa bwana harusi Misal Khan wakati akihojiwa kwenye eneo la tukio.

Kundi la ndugu wa bi harusi inasemekana liliongozwa na wajomba na binamu zake ambao walifanya mauaji hayo kwa madai ya kusafisha heshima ya ukoo wao.

Polisi walisema kwamba wamewakamata ndugu wa binti huyo na watu walioambatana nao kuwasaidia kufanya mauaji hayo.

Shirika la kutetea haki za binadamu limekuwa likipinga mauji yanayofanywa nchini humo kwa madai ya kulinda heshima ya familia.

Wanawake wanaobakwa au wanaopata mimba kabla ya ndoa wamekuwa wakiuliwa nchini humo kwa madai kwamba wanaitia aibu familia.

Mwaka 2005 rais wa wakati huo wa Pakistan, Pervez Musharaf aliamuru adhabu ya kifo kwa watu watakaofanya mauaji kwa madai ya kurudisha heshima ya familia zao.
[ Read More ]

Washabiki 12 Wa Michael Jackson Wajiua Kufuatia Kifo Chake


Msichana mmoja wa nchini Tunisia amejiua kwa kumeza vidonge kutokana na huzuni ya kifo cha Michael Jackson huku ikikadiriwa kuwa jumla ya washabiki 12 wa Michael Jackson kutoka sehemu mbali mbali duniani wameishajiua tangia kutangazwa kwa kifo chake. Msichana huyo wa mji wa El Manar uliopo kaskazini mwa Tunia alijiua kwa kunywa vidonge vingi sana baada ya kugubikwa na huzuni kubwa tangia habari za kifo cha Michael Jackson zilipotangazwa.

Taarifa zilizema kwamba msichana huyo alitumia siku nzima akiwa amejifungia chumbani kwake akiangalia video za Michael Jackson kabla ya kuamua kunywa vidonge hivyo na kufariki.

Michael Jackson alifanya shoo yake ya kwanza kabisa barani Afrika nchini Tunisia mwaka 1996 iliyohudhuriwa na washabiki wake 65,000.

Jumla ya watu 12 washabiki wakereketwa wa Michael Jackson kutoka sehemu mbali mbali duniani inasemekana wamejiua baada ya kutangazwa habari za kifo cha Michael Jackson.

Gary Taylor, rais na mmiliki wa tovuti ya MJJcommunity.com, iliyoanzishwa miaka kumi iliyopita alisema kwamba anavyofahamu hadi sasa washabiki 12 wa Michael Jackson ambao walihuzishwa sana na kifo chake wamejiua.

"Ninavyofahamu ni kwamba watu 12 wamejiua sehemu mbali mbali duniani, mmoja wapo ni raia wa Uingereza" alisema Taylor.

"Hali imekuwa mbaya, watu wanachukua uamuzi wa haraka ambao Michael asingetaka washabiki wake wauchukue, angewataka waendelee kuishi", alisema Taylor.

Jesse Jackson, rafiki wa karibu wa Michael ametoa video kwenye YouTube akiwataka washabiki wa Michael wasijidhuru.

Wakati huo huo taarifa za kutoka nchini Urusi zilisema kwamba mwanaume mmoja aliyejulikana kwa jina la Pável Talaláyev alijaribu kujiua muda mfupi baada ya kutangazwa kwa kifo chake na baada ya jitihada kubwa za madaktari kunusuru maisha yake alipozinduka alianza kuwalaumu madaktari kwa kumuokoa na kusema "Hili ni pigo kubwa sana kwangu, sitaki kuishi tena sijui kwanini wameniokoa nataka nikawe pamoja na Michael".
[ Read More ]

Kifo cha Michael Jackson: Uchunguzi zaidi waonyesha mambo ya kutisha


TAARIFA mpya za uchunguzi wa kifo cha msanii Michael Jackson zimeonyesha matokeo ambayo yanashangaza kwa kiasi kikubwa.

Vyombo mbalimbali vya habari ulimwenguni vimefichua kuwa msanii huyo alikuwa amedhoofika kiasi cha kutisha na kubakia mifupa kutokana na kutokula na kisha kutumia kiasi kikubwa cha vidonge.

Uchunguzi huo umeonyesha kuwa baada ya kifo chake mabaki ya baadhi ya vidonge hivyo yamekutwa tumboni mwake.

Mwili wake, uchunguzi huo umebaini kuwa ulikuwa umedhoofu kiasi kwamba kiuno, mapaja na mabega yake yalikuwa na matundo ya vidonda vingi vya sindano, vinavyodhaniwa kuwa ni vya sindano za kutuliza na kuondoa maumivu ambazo alichomwa mara tatu kutwa, tena kwa miaka mngi.

Pia, amekutwa na makovu mengi yaliyotokana na upasuaji wa mara 13 ailiofanyiwa kwa ajili ya kubadili sura yake.

Wataalam hao wamegundua uchunguzi wa kusikitisha wenye kuonyesha kuwa msanii huyo, Wacko Jacko hali yake ilikuwa imedhoofu wakati mauti yakimkuta wiki iliyopita mjini Los Angeles.

Uchunguzi huo umeonyesha kuwa licha ya kuwa na urefu wa futi tano na inchi 10, lakini msanii huyo alikuwa amepungua uzito na kubakia na kilo chache ambazo hazilingani na urefu wake.

Wataalam hao wanaeleza kuwa alikuwa akila mlo mmoja kutwa, kiasi kwamba wakati akifariki tumbo lake lilikuwa tupu, mabaki ya vidonge vilivyoanza kusagika ambavyo alitumia na sindano ambazo hatimaye zilisababisha moyo wake kusimama. Sampuli zaidi zimechukuliwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Kichwani, Wacko Jacko alikuwa amepoteza nywele karibu zote. Mfalme huyo wa pop, uchunguzi umeonyesha kuwa alikuwa akivaa nywele bandia, ambazo wachunguzi hawakuwa na kazi ya kuziondoa kwa ajili ya uchunguzi wao.

Kichwani mwake, upande wa sikio la kushoto, alikuwa na jeraha kubwa ambalo liliacha upara kutokana na ajali ya mwaka 1984 wakati alipoungua moto akipiga picha ya filamu ya tangazo la Kampuni ya Pepso.

Mwili mwake, wachunguzi hao wamebaini kuwa alikuwa amevunjika mbavu kadhaa, ikiaminika kuwa zilitokana na juhudi za kujaribu kuokoa maisha yake baada ya kuzimia. Matundu manne ya sindano yamegundulika karibu na moyo wa msanii huyo.

Uchunguzi huo umeonyesha kuwa harakati za kumwokoa ndizo zilizomsababishia madhara hayo yakiwamo ya sindano tatu zilizochomwa na kupenya ukuta wa moyo wake, kumsababisha madhara.

Katika uchunguzi huo, imeonekana kuwa magoti ya Jackson na sehemu ya mbele ya ugoko wake zilikuwa na majeraha kama ilivyokuwa mgongoni mwake.

Daktari wake binafsi, Conrad Murray, ambaye alikuwa karibu na msanii huyo amekamatwa na kuhojiwa huku familia ya msanii huyo ikieleza kuwa inataka uchunguzi zaidi unatakiwa kufanyika.

Dk Murray, ndiye anayeaminika kumpiga sindano msanii huyo kabla ya umauti kumkuta, akiaminika kumpa dawa iitwayo Demerol, jambo ambalo limemwingiza katika mzozo wa kitibabu.

Rafiki wa karibu wa familia, Mchungaji Jesse Jackson alieleza wasiwasi kuhusu chanzo cha kifo cha msanii huyo na kutaka uchunguzi zaidi na mtaalam, Dk Murray ambaye alikodiwa na Kampuni ya AEG Live , ambayo ilikuwa na jukumu la kuandaa matamasha 50 ya msanii huyo, katika ukumbi wa O2 Arena, London mwezi ujao, achunguzwe zaidi.

[ Read More ]

Profesa Haroub Othman afariki dunia


MHADHIRI mwandamizi wa Chuo Kikuu Cha Dar-es-Salaam, Professa Haroub Miraji Othman, 66, amefariki dunia usiku wa kuamkia jana katika hoteli ya Abuso Shangani mjini Zanzibar.

Kwa mujibu wa msemaji wa familia hiyo, Ali Uki alisema kifo cha Professa Othuman kilitokea ghafla akiwa usingizini. Alisema wakati mkewe akimuasha, alistuka alipoona Dk Othman haamki na ndipo alipoita watu kumsaidia.

Alisema mkewe pia aliomba msaada wa kuitiwa daktari ili aende kumpima na kuthibitisha kwamba taarifa za kuthibitisha kifo chake zilitolewa majira ya saa 1:30 asubuhi.

Professa Othman alifika mjini hapa juzi asubuhi akitokea Dar es Salaam kwa ajili ya kuhudhuria uzinduzi wa kitabu kilichotungwa na Professa Thomas Burgess, Ali Sultan Issa na Maalim Seif Sharif Hamad kiitwacho ‘Race Revolution and the Struggle for Human Rights in Zanzibar".

Hafla hiyo ilifanyika kwenye ukumbi mpya wa Al- Yamin Funguni mjini hapa na baadaye kuhudhuria uzinduzi wa Tamasha la Nchi za Jahazi (ZIFF) hadi majira ya saa 6:00 usiku baadaye kwenda hoteli ya Abuso iliyo Mji Mkongwe akiwa na mkewe Professa Saida Yahya Othman.

“Professa hakuwa anaumwa jana... si mlimuona alivyokuwa katika usinduzi wa kitabu asubuhi na usiku alikuwa katika uzinduzi wa tamasha la ZIFF. Amefariki alfajiri; kwa hakika kila mtu yatamfika mauti yeye ametangulia na sisi tupo nyuma yake ndio ameshatutoka, tunachofanya sasa ni kuwasiliana na jamaa kwa ajili ya matayarisho ya mazishi,” alisema msemaji huyo.

Makamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Professa Rwekaza Mukandala alisema Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimestushwa na kifo cha mhadhiri huyo na kumuelezea kuwa ni mtu asiyechoka na mchapakazi mzuri.

Profesa Othman atazikwa leo jioni na mipango ya mazishi inafanyika nyumbani kwake eneo la Baraste - Michenzani. Habari zinasema atazikwa pembeni kwa kaburi la mama yake mkoa wa Mjini Zanzibar.

Mhadhiri huyo atakumbukwa kwa msimamo wake na heshima aliyokuwa amejijengea kitaaluma katika sheria za kimataifa, masuala ya maendeleo na diplomasia.

Hakusita kuwakosoa viongozi wa serikali ya Jamhuri ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) wakati zilipokuwa zikienda kombo.

Mkuu wa Taasisi ya Mawasiliano ya Umma, Dk Bernadetta Killian alisema kuwa amestushwa na kifo cha mhadhiri mwenzake katika chuo kikuu cha Dar es Salaam.

Mgeni rasmi katika uzinduzi wa tamasha hilo la ZIFF alikuwa Waziri Kiongozi wa SMZ, Shamsi Vuai Nahodha na tamasha hilo lilikuwa likirushwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha serikali, TVZ.

Hadi mauti yanamfika, Professa Othman alikuwa mwenyekiti na muanzilishi wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ambacho kilianzishwa kwa ajili ya kutoa msaada wa kisheria kwa watu wenye kipato cha chini.

Mara baada ya kumaliza masomo yake ya juu nchini Urusi, Prof Haroub alirejea Zanzibar lakini hakupata ajira na kufanyiwa mipango na serikali kwenda kufanya kazi Bara.

Professa Othman alikuwa akifanya kazi katika kitivo cha sheria cha UDSM kuanzia miaka ya sabini na amefariki akiwa mhadhiri mwandamizi.

Mbali na elimu yake, Professa Othman alikuwa mstari wa mbele katika kupigania haki na ameshawahi kuteuliwa katika tume mbalimbali, ikiwemo ya kufanya marekebisho ya katiba na tume ya Nyalali.

Tume ya Nyalali ilikuwa ikiangalia mfumo unaofaa kisiasa nchini wakati dunia ikiwa kwenye mageuzi ya kisiasa na kiuchumi baada ya kumalizika kwa vita baridi kati ya mataifa ya mashariki na magharibi. Aliwahi kuwa mwenyekiti wa bodi ya iliyokuwa Shirika la Habari la Tanzania (Shihata) katika mwaka 1995.

Katika kipindi cha uchaguzi mkuu wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi, Prof Othman alikuwa mwenyekiti wa taasisi ya wangaalizi wa ndani wa uchaguzi ambayo iliingia katika lawama kubwa baada ya kusema uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa mwaka 1995 haukuwa huru na haki jambo ambalo lilimsababishia kuwekewa chuki na baadhi ya viongozi wa Zanzibar kutokana na msimamo huo.

Waangalizi waliokuwa chini ya Professa Othman walitoa taarifa ya kwamba uchaguzi mkuu wa mwaka 1995 haukuwa huru na haki tofauti na taarifa ya Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC).

Mwezi uliopita alihudhuria semina iliyowakutanisha waandishi wa habari waandamizi kuhusu jinsi ya kuhakikisha chaguzi zinazofuata zinakuwa huru na haki bila ya kutawaliwa na fujo pamoja na kutoa mafunzo ya sheria za kimataifa na haki za binaadamu kwa makamanda na wakuu vya vyuo vya mafunzo Zanzibar, ikiwa ni hatua moja ya kuwaelimisha juu ya masuala ya ukiukwaji wa haki za binaadamu.

"Nikiwa hai inshaallah nataka kushuhudia uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 unafuata misingi yote ya demokrasia na haki za binadamu, zaidi kwa vyombo vya habari," alisema Prof Othman katika semina hiyo.

Akizungumzia kifo hicho, Mwanadiplomasia Dk. Salim Ahmed Salim na katibu mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad walieleza kupokea taarifa hizo kwa mshituko mkubwa na kwamba msomi huyo atakumbukwa kwa mengi, lakini wakasema kubwa zaidi ni utetezi wake kwa wanyonge na kupigania haki za binaadamu.

Naye Prof Abdallah Safari alisema amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha msomi huyo na kuelezea kifo chake kuwa ni msiba mkubwa kwa wanataaluma na jamii kwa ujumla.

"Unajua pengo la Prof Haroub ni kubwa na si kirahisi kuzibika katika Chuo kikuu cha Dar es Salaam kwa sababu kifo cha mwanataaluma siku zote pengo lake huwa kubwa sana," alisema Profesa Safari.

Alimfananisha Prof Haroub na wanafalsafa wa zamani kama Walter Rodney, aliyeandika kitabu kinachoelezea jinsi Ulaya ilivyorudisha nyuma maendeleo ya kiuchumi ya Afrika, na kwamba dunia imempoteza mwanadiplomasia mkubwa.

"Kwa Tanzania ukitaka uchambuzi mzuri wa migogoro hususan ya Mashariki ya Kati, Afrika na nchi nyingine, basi bila ya kumpata Profesa Haroub ni vigumu kupata uchambuzi uliokamilika," alisema.

Alisema hii ni wiki ya misiba mikubwa kwa sababu Tanzania imempoteza Sheikh Suleiman Mohamed Gorogosi, aliyefariki kwa ajali ya gari na mwanamuziki nyota wa miondoko ya pop, Michael Jackson wa Marekani.

Alimkumbuka Prof Othman wakati alipofundisha katika miaka ya sabini akiwa UDSM na kuelezea kuwa walikuwa na uhusiano mzuri.

Prof Othman alikuwa mstari wa mbele kuikosoa SMZdhidi ya ukandamizaji na ukiukwaji wa haki za raia.

Prof Othman ameacha mjane ambaye ni Professa Saida Othman na mtoto mmoja, Tahir Othman.

[ Read More ]