Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

Wahasibu watakiwa kuwania CPA

Wahitimu wa Uhasibu na Fedha wa Chuo Kikuu Mzumbe (MU), wameshauriwa kujiendeleza kwa kufanya mitihani ya juu ya Uhasibu (CPA) na baadaye kusajiliwa katika Bodi ya Uhasibu (NBAA) ili watambulike wanataaluma.

Changamoto hiyo ilitolewa na Meneja wa Mfuko wa Pensheni wa Mashirika ya Umma (PPF), Kanda ya Mashariki na Kati, Meshack Bandawe, wakati wa hafla maalumu ya wanafunzi wanaotarajia kumaliza masomo yao ya Stashahada na Shahada.

Alisema taaluma ya uhasibu ni moja ya taaluma zinazohitaji kuwa na uaminifu na uadilifu wa kiwango cha juu kutokana na mazingira ya kazi yaliyojaa vishawishi vingi zaidi ukilinganisha na kazi nyinginezo.

Kwa mujibu wa Meneja huyo wa PPF Kanda ya Mashariki na Kati, wapo watu wenye taaluma ya uhasibu ambao wamekuwa wakiharibu sifa ya taaluma hiyo na kusababisha wananchi kupoteza imani.

Hivyo alisema ni wajibu wa wanafunzi wa chuo kikuu hicho kuheshimu sheria za kazi kwa kuwa waadilifu ili kuepukana na sifa mbaya katika utendaji wao kwa siku za usoni pindi watakapopata ajira.

Alisema watakapoingia kwenye ajira iwe ya sekta binafsi ama ya umma, wana wajibu wa kusimamia na kuhakikisha michango ya wanachama wa mifuko ya jamii ukiwamo wa PPF inawasilishwa kwa wakati ili kuepukana usumbufu baada ya watumishi kustaafu kazi ama kuondoka kwa sababu yoyote.
[ Read More ]

Dereva wa teksi ashikiliwa kwa gari kutumika katika ujambazi

Polisi mkoani Singida inamshikilia dereva teksi kwa kosa la gari lake kuhusika na uporaji wa fedha Sh milioni nne mali ya mfanyabiashara wa alizeti, na baadaye kuvamia baa ya Kairo mjini hapa, na kutoweka na mauzo ya siku nzima.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani Singida, Celina Kaluba matukio hayo yalitokea Jumanne na Jumatano wiki iliyopita katika eneo la Kibaoni na Mitunduruni katika Manispaa ya Singida.

Alimtaja mtuhumiwa huyo kuwa ni Said Juma (28) mkazi wa Majengo mjini hapa ambaye ni dereva anayeendesha teksi yenye namba za usajili 749 ABU na ubavuni ikiwa na namba 241. Alisema dereva huyo akiwa na wenzake ambao wanaendelea kutafutwa, wakiwa na silaha mbalimbali walifika nyumbani kwa mfanyabiashara Ruben Mhai (30) na kupora kwa nguvu Sh milioni nne zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye mkoba.

Kamanda huyo wa polisi alisema kabla ya kufanikisha unyang'anyi huo, Pendaeli Salumu (40) alijeruhiwa vibaya kwa kukatwa panga sehemu mbalimbali za mwili wake, huku mlinzi wa nyumba Rajabu Salumu (38) akivunjwa mkono wa kushoto.

Alisema baada ya uhalifu huo, wezi hao wakiwa na gari hilo hilo, Jumatano walivamia tena baa ya Kairo iliyopo Mtaa wa Mitunduruni na kupora mauzo ya siku nzima ambayo hata hivyo kiasi chake hakijafahamika hadi sasa.

Alisema watuhumiwa wanatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote upelelezi utakapokamilika. Katika tukio la tatu, Kaluba alisema wanamsaka dereva teksi Richard Ngoi baada ya kutoweka na gari hilo lenye namba za usajili T777 AAE Toyota mali ya Mary Mashuda (60) mkazi wa Mtaa wa Kibaoni.

Dereva huyo anadaiwa kutoweka na gari hilo Jumanne iliyopita wakati tajiri yake akiwa ndani ya Benki ya NMB kupatiwa huduma za kifedha, na alipotoka hakumwona tena mfanyakazi wake.

Kutokana na tukio hilo, Kaluba alisema wanamshikilia fundi magari wa gereji maarufu mjini hapa 'Vijana Garage,' Peter Mlay (25) kwa madai ya kushiriki wizi huo wa gari, na upelelezi unaendelea.
[ Read More ]

SMZ yashutumu wahasibu wa kigeni kwa ukwepaji kodi

Wizara ya Fedha na Uchumi Zanzibar imewatuhumu wahasibu wa kigeni wanaofanya kazi nchini kwa kushirikiana na wawekezaji kukwepa kulipa kodi na hivyo kuikosesha serikali mapato.

Akizungumza katika ufunguzi wa semina kwa jumuiya ya wahasibu na wakaguzi wa hesabu iliyofanyika jana mjini hapa, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Uchumi, Abdi Khamisi Faki alisema zipo dalili zinazoashiria kuwa wahasibu hao hushirikiana na waajiri wao kufanya udanganyifu katika suala la kulipa kodi katika sekta mbalimbali ikiwamo hoteli za kitalii.

Alisema kutokana na kukithiri kwa vitendo vya ukwepaji wa kodi kwa baadhi ya wawekezaji wakishirikiana na wahasibu wa kigeni wanaowaajiri, serikali imekuwa ikikosa mapato, jambo linaloiathiri nchi kiuchumi na kusababisha hasara kubwa kwa taifa.

“Tuna idadi kubwa ya wahasibu kutoka nchi jirani wanaokuja kutafuta ajira na tuna mashaka kuwa wanashirikiana na wawekezaji wanaowaajiri kudanganya kulipa kodi,” alisema Faki huku akisisitiza kuwa serikali inafanya jitihada kukomesha suala hilo.

Alisema serikali inatafakari hatua za kuchukua juu ya suala hilo ikiwamo kuangalia uwezekano wa kuzuia ajira kwa wahasibu wa kigeni katika sekta hizo na badala yake ajira hiyo ifanywe na wazalendo tu.

Alisema kuwapo kwa wafanyakazi wazalendo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kutatua tatizo hilo kwa kuwa itakuwa rahisi kwao kuweka maslahi ya taifa mbele na pia kutaongeza ajira kwa vijana wa Zanzibar na kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira kwa vijana.

“Hivi sasa serikali inaangalia uamuzi wa kuchukua juu ya tatizo hili, ikiwemo kuzuia ajira kwa wahasibu wa kigeni kwa kuwa ndio chanzo kikuu cha kukithiri kwa vitendo vya ukwepaji wa kodi nchini,” alisema.

Semina hiyo iliyowashirikisha wahasibu kutoka taasisi mbalimbali iliandaliwa na jumuiya ya wahasibu na wakaguzi Zanzibar kwa lengo la kuwaongezea uwezo wafanyakazi wa taaluma hiyo na kuwakumbusha wajibu wao.
[ Read More ]

Nusu ya wajawazito Singida wanajifungulia majumbani

Zaidi ya asilimia 50 ya wanawake wajawazito mkoani Singida hujifungulia majumbani na kwa wakunga wa jadi, hali inayohatarisha usalama wa maisha yao na watoto wanaozaliwa. Hayo yalibainishwa na daktari bingwa wa magonjwa ya wanawake na uzazi Mkoa wa Singida, Dk. Christopher Mgonde kwenye mafunzo ya kuokoa maisha ya mama na mtoto wakati wa kujifungua.

Dk. Mgonde alisema ingawa takwimu zinaonyesha kuwa idadi ya vifo vya wanawake wakati wa kujifungua mkoani Singida imepungua kutoka 61 mwaka juzi hadi 49 mwaka jana, lakini bado kuna tatizo kubwa la wajawazito wengi kutojifungulia kwenye vituo vya tiba.

Alisema miongoni mwa mambo yanayosababisha hali hiyo ni umbali mrefu kwenda kwenye zahanati, vituo vya afya na hospitali, mila na desturi na matusi kutoka kwa baadhi ya watoa huduma.

Alisema pamoja na mambo mengine ikiwamo elimu duni na matatizo ya kiuchumi, hizo ndizo sababu kuu zinazosababisha wengi wa wanawake kuhudhuria vizuri kliniki wakati wa ujauzito wao na kujifungulia majumbani badala ya vituo vya tiba. Dk. Mgonde alisema katika kukabiliana na tatizo hilo, Idara ya Afya kupitia vitengo vyake mbalimbali inaendelea kutoa elimu kwa akinamama juu ya umuhimu wa kujifungulia kwenye vituo vya tiba.

Alisema lengo la hatua hiyo ni kupunguza kiwango cha vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua ili kulinda kizazi na ustawi wa jamii kwa ujumla. Mafunzo hayo ya wiki mbili kwa watoa huduma za uzazi yameandaliwa na kuratibiwa kwa pamoja na Idara ya Afya Mkoa wa Singida na Taasisi ya Benjamin William Mkapa.
[ Read More ]

Watumishi Mahakama Kisutu waomba ulinzi

Watumishi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wameiomba Serikali kuimarishia ulinzi katika eneo la mahakama hiyo na wao binafsi. Maombi hayo yalitolewa jana na watumishi hao, mbele ya Waziri wa Sheria na Katiba, Mathias Chikawe, alipotembelea mahakama hiyo. Akizungumza kwa niaba ya watumishi hao, Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Addy Lyamuya, aliiomba serikali kupitia kwa Chikawe, kuwaimarishia ulinzi watumishi wa mahakama hasa ikizingatiwa uzito wa kesi zinazosikilizwa hapo. Lyamuya alisema watumishi hao wanahitaji ulinzi huo wanapokuwa kazini na hata nyumbani, ili kudhibiti jambo lolote la hatari litakalowakumba.

Aliongeza kuwa, Jeshi la Polisi linatakiwa kuboreshwa, ili lifanye kazi ndani na nje ya mahakama huku changamoto kubwa ikiwa ni ya kukosa vitendea kazi vitakavyowasaidia kuimarisha ulinzi. Lyamuya alimwambia Chikawe kuwa mbali na matatizo hayo, mahakama ina mazingira duni ambayo ndiyo yanayotegemewa kusikilizia kesi hizo. Akisoma taarifa ya maendeleo ya mchakato wa utenganishaji wa shughuli za mashtaka na upelelezi katika mahakama hiyo, Msaidizi wa Mkurugenzi wa Mashtaka, Winfrida Kasoro, alisema mchakato umeleta mafanikio mengi ikiwa ni pamoja na uharakishwaji wa kesi mahakamani hapo.

Aliongeza kuwa mbali na mafanikio hayo, mchakato huo umepata changamoto nyingi kama kutopatikana mashahidi kwa wakati na mawakili kuacha kazi kutokana na kipato kidogo. Akijibu hoja zilizowasilishwa katika kikao hicho, Chikawe alisema atawasilisha matatizo hayo katika ngazi husika na pia aliishauri mahakama kuandika barua ya maombi ya kukarabatiwa kwa jengo hilo. Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kuajiri wanasheria wapya, ili kukabiliana na utandawazi ikiwa ni pamoja na kuongeza kipato cha wafanyakazi wa mahakama.
[ Read More ]

Kortini wakitaka kuiba Sh bilioni 6 za Stanbic

Watu wawili wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, wakikabiliwa na mashitaka ya kula njama za kutaka kuiba zaidi ya Sh bilioni 6 mali ya Benki ya Stanbic. Akisoma mashitaka jana mbele ya Hakimu Nyigumalila Mwaseba, Mwendesha Mashitaka, Epifras Njau, alidai kuwa washitakiwa hao walikula njama za udanganyifu ili kutaka kuiba kiasi hicho cha fedha, jambo ambalo ni kinyume na sheria ya nchi.

Watuhumiwa hao walitajwa kuwa ni Kunji Meena (29), mfanyabiashara na mkazi wa Kurasini na Tumsifu Kimaro(33), dereva na mkazi wa Kurasini Shimo la Udongo, Dar es Salaam. Njau alidai kuwa, kati ya Mei 16 na 17 mwaka huu, watuhumiwa hao pamoja na wenzao ambao hawajafikishwa mahakamani, walikula njama za wizi Stanbic tawi la Sukari House. Aidha, alidai kuwa Meena anakabiliwa pia na tuhuma zingine mbili za wizi wa Sh 800,000 mali ya Tumsifu Kimaro ambaye ni mtuhumiwa wa pili katika kesi ya kwanza.

Njau alidai mbele ya Mwaseba kuwa kati ya Mei 16 na 17 mwaka huu, mtuhumiwa akitumia kadi ya ATM namba 0140518196401 alichukua Sh 400,000 siku ya kwanza na kiasi hicho hicho siku ya pili katika tawi hilo. Washitakiwa wote walikana mashitaka yao na wako nje baada ya kutimiza masharti ya dhamana zilizowataka kuwa na wadhamini wawili ambao ni wafanyakazi wa Serikali au taasisi zinazotambulika na ahadi ya Sh 500,000 kila mmoja, kesi hiyo inatarajiwa kutajwa mahakamani hapo Juni 8 mwaka huu.
[ Read More ]

Majambazi waua askari 2 Zanzibar

Askari wawili wa Kikosi cha Valantia kinachomilikiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), wameuawa na majambazi wakati wakilinda kituo cha mafuta cha Mwanakwerekwe mkoa wa Mjini Magharibi kisiwani Unguja. Askari waliouawa ni Taibani Mikidadi Ali (23) na Juma Mcha Ali (25) ambao walijeruhiwa na majambazi hao kwa risasi kichwani na kifuani.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Bakari Khatib Shaaban, alikiri jana kutokea kwa tukio hilo saa mbili usiku juzi, baada ya majambazi kuvamia kituo hicho kwa lengo la kupora fedha. Katika purukushani hizo, majambazi hao walifyatua risasi na kuwaua walinzi wawili wa Valantia waliokuwa wakilinda kituo kinachomilikiwa na kampuni ya Zanzibar Petroleum. Katika tukio hilo, majambazi hao walipora silaha aliyokuwa nayo mmoja wa walinzi hao, ikiwa na risasi 10. Jeshi la Polisi linamshikilia Gideon Simponda kwa uchunguzi baada ya kukiri kumiliki gari namba ZNZ 634 ambalo lilitumika katika tukio la ujambazi.

“Kwa sasa, Jeshi la Polisi linamshikilia Gideon Leonard Simponda kwa uchunguzi zaidi...yeye alijitokeza na kusema anamiliki gari ambalo liliporwa na baadaye kutelekezwa,” alisema Kamanda Shaaban. Aidha, polisi waliipata silaha iliyoporwa na majambazi hao aina ya Rifle yenye risasi 10. Kamanda alisema hata hivyo majambazi hao hawakuondoka na fedha ila walimjeruhi Bilali Omar ambaye alikuwa mpita njia eneo hilo, na amelazwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja kwa matibabu. Askari wa vikosi vya SMZ hutumiwa kulinda vituo mbalimbali vya mafuta na taasisi nyingine za watu binafsi zikiwamo benki.
[ Read More ]

CCM YAIBUA USHINDI BUSANDA


Mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Lolesia Bukwimba, ametangazwa kuwa Mbunge Mteule wa Jimbo la Busanda, baada ya kuwashinda wagombea wa vyama vingine vilivyokuwa vikishiriki uchaguzi huo mdogo wilayani Geita.

Mgombea huyo alitangazwa jana kwa kupata kura 29,242 wakati Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambacho hata hivyo kiliyakataa matokeo, kilishika nafasi ya pili kwa kupata kura 22,799. Chama cha Wananchi (CUF) kilichopata kura 977 na cha United Democratic (UDP) chenye kura 271, ‘viliingia mitini’ baada ya wagombea na mawakala wake kutoshiriki mchakato wote wa kuhesabu na kuhakiki kura katika hatua za mwisho.

Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi, Dani Mollel, alisema idadi ya waliojiandikisha kupiga kura walikuwa 135,163, na waliopiga kura ni 55,660, kura halali zikiwa 53,309 na zilizoharibika 2,069. Kabla ya kutangaza matokeo hayo, msimamizi huyo wa uchaguzi aliwaita wagombea wawili waliokuwapo ambao ni Bukwimba na Finias Magesa, kujaza fomu maalumu ya matokeo baada ya kupata takwimu sahihi na kuyathibitisha kabla ya kuyatangaza.

Hata hivyo, wakala wa Chadema, Basil Lema, alisimama na kueleza kwamba mgombea hatasaini fomu hizo, hadi hapo watakapopewa nafasi wagombea na mawakala wao kutoa maoni juu ya mchakato mzima wa uchaguzi na wa kuhesabu kura. Msimamizi wa uchaguzi alifafanua, kwamba hatua hiyo ilifanyika tangu asubuhi baada ya wajumbe wa kikao hicho cha kuhesabu kura kukaa kwa muda mrefu wakiwasubiri wagombea na mawakala wa vyama vingine tofauti na CCM, ikiwamo Chadema, bila kuonekana.

Kutokana na kwamba awali msimamizi huyo alishatoa ufafanuzi juu ya kilichofanyika mbele ya wakala mwingine wa Chadema, Benson Kigaila kabla ya Lema kuingia ukumbini hapo saa 7 mchana huku amechelewa, baadhi ya watu waliokuwa ukumbini walilazimika kuingilia kati kwa kusisitiza kwamba uamuzi wa msimamizi ulifuata sheria. Baada ya majibizano yaliyochukua dakika kadhaa yakihusisha baadhi ya wawakilishi wa CCM na mawakala hao wa Chadema, msimamizi aliamua kumtangaza Bukwimba kuwa mbunge mteule na akataka yeyote mwenye malalamiko, afuate utaratibu wa kujaza fomu maalumu, jambo ambalo mgombea huyo wa Chadema alilifanya.

Kulingana na maelezo yaliyokuwa yametolewa awali kabla ya Lema kuwasili ukumbini, Msimamizi alitoa ufafanuzi kwa wajumbe wa kikao hicho ambacho waandishi waliruhusiwa kuingia na kusikiliza, kwamba mgombea na wakala wa Chadema walifika wamechelewa, hali ambayo iliathiri mchakato wa kutangaza matokeo. Msimamizi Mkuu wa Uchaguzi, Mollel, alimfafanulia Kigaila kwamba vyama vyote vilitaarifiwa tangu Mei 15 mwaka huu, kwamba Mei 23 na 24 wakutane katika ofisi hizo za halmashauri ya wilaya kwa ajili ya kuhesabu kura, lakini wahusika (kasoro wa CCM), hawakuonekana na mtandao wa mawasiliano yao haukupatikana.

“Nikapiga kwa wajumbe wa UDP, hawakupatikana. Wiki iliyopita, wajumbe wa Chadema niliwasiliana nao sana kwa mtandao, lakini kipindi hiki (baada ya uchaguzi) wameadimika,” alisema Mollel. Akisisitiza namna alivyovihimiza vyama kushiriki mchakato huo wa kuhesabu kura, msimamizi huyo alisema pia Mei 23 mwaka huu, aliandika barua kwa makatibu wote wa vyama kuwakumbusha waje. Alisema juzi usiku, baadhi walifika akiwamo Mohamed Habib Mnyaa wa CUF ambaye hata hivyo aliondoka saa 7 usiku na kuwaacha wajumbe wengine wakiendelea na mchakato huo hadi saa 12 alfajiri.

Alisema alipompigia Mnyaa, alimwambia endeleeni hali ambayo alisema ilidhihirisha kwamba aliridhishwa na kilichokuwa kikiendelea. Kwa mujibu wa Mollel, baada ya kuona hali hiyo ya wagombea na mawakala kutofika, ilimlazimu kupiga simu kwa Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Rajabu Kiravu, ili kupata mwongozo wa nini kiendelee; akajibiwa kuwa hakuna sababu ya kuahirisha kama matokeo yote yamekamilika. “Mkurugenzi akashauri niwakumbushe wajumbe kwa barua na dispatch na akasema ikishapokewa, endeleeni na kikao.

Tukaendelea bila wawakilishi,” alisema msimamizi huyo wa uchaguzi. Akifafanua sababu za kikao hicho kuendelea bila mawakala, Mollel alisema walizingatia kwamba matokeo hayo yalitoka katika vituo ambavyo vyama husika vilikuwa na mawakala na akasema kwa kuchukua uamuzi huo, hawakuvunja sheria. Alisisitiza katika kikao hicho kwamba, “huu si uamuzi wa kuzuia wenzetu kushiriki. Uamuzi ulikuwa halali. Uamuzi sikuufanya kugandamiza chama, bali tumefuata taratibu na ndio wenzetu wakatokea (akimaanisha wa Chadema).”

Kwa upande wa Chadema, Lema na Kigaile walikiri kupokea taarifa ya kuwataka washiriki mchakato huo wa kuhakiki kura, lakini wakasema hawakuelezwa muda wa kufika katika ofisi hizo za Halmashauri ya Wilaya ya Geita kwa ajili ya kazi hiyo. Wakati msimamizi wa uchaguzi, Mollel katika taarifa yake ya awali alisema mchakato huo ulianza usiku wa kuamkia juzi hadi jana alfajiri, kwa upande wa mawakala hao wa Chadema, walidai kwamba walifika katika eneo hilo saa 5 asubuhi kwa kuwa hawakuambiwa muda halisi.

Akizungumza na waandishi wa habari juu ya uamuzi wa kukataa matokeo hayo, mgombea wa Chadema alisema uchaguzi haukuwa huru kutokana na mazingira yaliyojitokeza wakati wa kampeni. “Zoezi hili liligubikwa na matatizo yanayokiuka misingi ya utawala bora,” alisema Magesa na kuyataja matokeo hayo kuwa ni ya NEC na CCM na kwamba si ya wananchi wa Busanda. Akikariri idadi ya watu 79,703 ambao hawakupiga kura, Magesa alisema Chadema walilalamika tangu wakati wa kampeni juu ya vitendo vya ununuzi wa shahada, lakini NEC ilipuuza kilio chao.

Magesa ambaye aliomba fomu maalumu ya malalamiko kwa ajili ya kuijaza, alidai kulikuwa na vitendo vya ugawaji chumvi, vitisho kwa wapiga kura na pia akalalamikia hatua ya Serikali kuanza mchakato wa kuweka nguzo za umeme katika barabara iendayo kata ya Kamena wakati wa mchakato wa uchaguzi. Wakati huo huo, nderemo na vifijo zilitawala kabla na baada ya mgombea wa CCM kutangazwa kushinda. Kwa upande wa mgombea wa Chadema, Magesa, alionekana mnyonge ndani ya ukumbi wa kuhesabia kura huku akiwa amesindikizwa na watu watatu, tofauti na ilivyotarajiwa.

Mmoja wa viongozi wake, Tundu Lisu, siku ya kuhitimisha kampeni (Jumamosi iliyopita) aliwahimiza wafuasi wake wasikose katika ofisi hizo za halmashauri kushuhudia mchakato wa matokeo, lakini hali ilikuwa tofauti jana kutokana na mgombea wao kujitokeza akiwa na wafuasi wachache bila viongozi wa juu wa chama hicho waliokuwa wakimnadi wakati wa kampeni. CUF ambayo katika Uchaguzi Mkuu wa 2005 ilikuwa ya pili kwa mgombea wake kupata kura 26,000, safari hii imedorora na kuiachia Chadema kutamba ambayo mwaka 2005 ilipata kura 3,000 katika jimbo hilo.
[ Read More ]