Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

UKATILI: MAITI ZA VITOTO 11 ZAFUKULIWA SHIMO MOJA.

-
Rehema Mwinyi.

KATIKA hali isiyo ya kawaida, wakazi wa Mwananyamala Kwakopa, jijini Dar es Salaam wamepatwa na mshituko mkubwa baada ya kaburi moja kugundulika jana (Jumatatu) likiwa na watoto 11 waliozikwa ndani yake, tukio lililoelezwa kuwa ni ukatili wa kutisha, Uwazi lina habari kamili.

Habari zilizolifikia gazeti hili jana zilieleza kuwa mkazi mmoja wa eneo hilo aliyefahamika kwa jina moja la Thabiti  ndiye aliyeligundua kaburi hilo alipokuwa  akitafuta sehemu ya kuchimba jalala, jirani na Hospitali ya Mwananyamala.
Ilielezwa kuwa mzee huyo alipofika eneo hilo alishtuka baada ya kuona nzi wengi wamezingira huku kukiwa na harufu kali, machale yakamcheza na kuhisi kuwa huenda kuna kitu kibaya kimefukiwa.

“Mzee Thabiti aliamua kuwataarifu polisi ambao walifika eneo la tukio, jirani na makaburi ya Mwananyamala. Baada ya kuona hali ilivyokuwa, polisi waliwapigia simu madaktari waliowasili muda mfupi baadaye,” kilieleza chanzo chetu.

POLISI KUFIKA ENEO LA TUKIO
Habari zinaeleza kuwa mara baada ya polisi kupewa taarifa hizo na kuwasili eneo la tukio wakiwa kwenye gari aina ya Landrover ‘defender’ walianza uchunguzi wao mara moja.
Mwandishi wetu aliyekuwepo eneo la tukio, alishuhudia kazi ya kufukua kaburi hilo ikifanywa kwa uangalifu mkubwa.

Dakika chache baadaye  shimo likiwa na urefu wa futi nne, lilionekana shuka jeupe likiwa limeviringishwa kitu. Lilipotolewa, kwa mshangao mkubwa maiti ya kitoto kichanga ikadondoka.

Polisi aliyekuwa akifanya kazi hiyo alipolichunguza vizuri shuka lile, aligundua kuwa kuna kitu kingine kimebaki. Alipoingiza mkono, alichomoa maiti nyingine ya kitoto kichanga.

KANGA KIBAO ZILITUMIKA
Askari huyo aliendelea na zoezi hilo na baadaye akalifunua kabisa shuka hilo, ndipo alipokuta maiti nyingine za watoto wachanga zikiwa zimevingirishwa kwenye kanga tofauti. 
Zilipohesabiwa ilibainika kuwa jumla ya maiti 11 zilikuwa zimefukiwa kwenye kaburi hilo.

Uchunguzi zaidi ulibaini kuwa moja ya kanga iliyokutwa kwenye kaburi hilo ilikuwa imebandikwa plasta yenye maneno yaliyosomeka: ‘Ruth Mtanga, Male Pre-mature (yakimaanisha kuwa mwanamke mwenye jina hilo alikuwa amejifungua ‘njiti’ wa kiume).

Haikufahamika maandishi yale kwenye plasta hiyo yameandikwa na nani katika hospitali gani, hivyo polisi wakaanzia uchunguzi wao hapo.
Uchunguzi wa gazeti hili eneo la tukio ulibaini kuwa shuka lililotumika kuviringishia maiti za watoto hao lilikuwa imeandikwa Mwananyamala.

DAKTARI AKACHA WANAHABARI
Daktari mmoja wa Hospitali ya Mwananyamala aliyefahamika kwa jina moja la Karamahia, alipohojiwa kuhusiana na shuka hilo pamoja na maiti za watoto hao wachanga, alikataa kusema chochote kwa madai kuwa tayari sakata hilo lipo mikononi mwa polisi.

Polisi waliondoka na miili hiyo kuelekea Hospitali ya Mwananyamala, ilikoenda kuhifadhiwa wakati uchunguzi wa kina ukiendelea. 
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi wa Kinondoni, Charles Kenyela alipohojiwa na gazeti hili jana, alisema taarifa hizo amezipata na anazifanyia kazi hivyo apewe muda.

WANANCHI WALIVYOSIKITISHWA
Hata hivyo, baadhi ya wananchi walioshuhudia tukio hilo waliliambia Uwazi kwa masikitiko kuwa kitendo hicho siyo cha kibinadamu na ni tukio la kwanza la kutisha kugundulika hapa nchini.
“Haya mambo ya binadamu kuzikwa kaburi moja tulikuwa tukiyasikia kwa wenzetu lakini sasa tumeyashuhudia hapa leo. Haya ni mambo ya kutisha,” alisema shuhuda mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja la Zuwena.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwa watoto hao  hawakuzikwa siku nyingi zilizopita kwa sababu walikuwa bado hawajaharibika sana.



source-global publisher

2 Responses so far.

  1. Anonymous says:

    HAKIKA ALLAH AWAWEKE HAO WATOTO ROHO ZAO MAHALA PEMA PEPONI WANGEKUWA WAZIMA NINGEWAOMBA WANIPE JAPO WATOTO WAWILI NIWALEE MAANA KUNA WATU WANATAFUTA WATOTO WA KULEA HAWAPATI

  2. Anonymous says:

    kwa kweliinasikitisha sana,huwezi kuamini kama watu wangeweza kufanya unyama kiasi hii,dunia imekosa huruma kwa kweli.

Leave a Reply