Banner 468

1234453_10201664080105694_1716282793_n
Facebook

Aanguka na Kujifungua nje ya Wodi

-
Rehema Mwinyi.

MAMA mmoja anaetambulika kwa jina la Mwantatu Kombo mkaazi wa Miembeni ameelezea kusikitishwa kwake kwa kitendo alichofanyiwa na wauguzi wa hospitali ya Mnazimoja wodi ya wazazi wakati alipokwenda kumpeleka jamaa yake kwa ajili ya kujifungua.

Akisimulia mkasa huo Mwantatu alisema kuwa tukio hilo lilitokea wiki iliyopita majira ya saa 9 usiku, ambapo alifika hospitalini hapo kwa lengo la kumpeleka jamaa yake na hatimaye kujifungua nje ya wodi ya wazazi hospitalini hapo.

Alisema alipofika wodini hapo akiwa amefuatana na mjamzito huyo, anaejulikana kwa jina la Fatma Ali Suleiman ambaye alimuomba ampatie msaada wa kumpeleka hospitali, lakini hakupokelewa kutoka na kutokuwa na vifaa.


Alisema kutokana na kutokuwa na vifaa, aliambiwa na wauguzi hao atoke nje na hawatompokea mjamzito huyo pamoja na kuwaeleza kuwa atavilipia baada ya kujifungua kutokana na hali yake.

Pamoja na Mwantatu kudai kuwafahamisha yote hayo kuhusu mzazi wake lakini madaktari hao hawakumsikiliza kilio chake na kumtaka atoke nje yeye na mjamzito wake huku mzazi huyo akiwa na uchugu na tayari kwa kujifungua.

"Wakati nikiwa natoka nje na mjamzito wangu, alianguka mbele ya wodi ya wazazi na kujifungua hapo hapo chini, mara baada ya kujifungua nilirudi kwa wauguzi kuwambia mgonjwa wangu ameshajifungua nje naomba kuomba msaada lakini pia walikataa.

Kwa upande wake Mzazi huyo Fatma Ali alisema kuwa mwanzo wa kupata ujauzito huo alikwenda kupima na kuambiwa atoe shilingi 10,000 kwa ajili ya kununua gamba na hali yake alikuwa hana hata shilingi na ndipo akaondoka na kwenda zake hadi kujifungua kwake.

Kwa upande wake Msaidizi Katibu hospitali ya Mnazimmoja Mohammed Nadi alithibitisha kutokea tukio hilo kwa madaktari hao na alisema kitendo walichokifanya wauguzi kwa kumuacha mzazi kujifungua nje ya wodi si kitendo cha kiungwana.


Akizungumzia kadhia hiyo Katibu wa Hospitali ya Mnazimmoja, Omar Abdalla Ali, aliwashauri wananchi wanapofanyiwa vitendo vya udhalilishaji wawe na utaratibu wa kuripoti kwa ushahidi wa kutosha pamoja na kufika katika vyombo vya sheria kwa ajili ya hatua za kisheria zaidi.

"Mara baada ya tukio hilo tuliwaandikia barua na kutaka wajieleze lakini hatukuridhika na maelezo yao waliyoyathibitisha kwenye barua yao, hivyo nitawaita kwenye kamati ya maadili wiki ijayo kwa ajili ya kusikiliza pande zote mbili na kulichukulia hatua za kisheria zinazofaa”, alisema Msaidizi huyo.

Aidha aliwataka madaktari kuachana na vitendo vya rushwa ambapo hivi sasa vimeonekana kukithiri kwa kiasi kikubwa na kupelekea kutothamini utu na binadamu.

Barua yenye ripoti kutoka kwa Muuguzi wa Maternity Ward ya Februari 2 mwaka huu, imeeleza kwamba siku ya tarehe saba mwezi huu wauguzi wawili (majina tunayahifadhi) walimpokea mgonjwa vizuri na wamemuweka katika kochi na kabla hawajamchunguza walimtaka atowe vifaa vyake, jamaa zake walijibu hawana na walielekezwa wakanunue hospitali ya Al-Rahma.
Ripoti hiyo imeongeza kuwa walidai hawana pesa, wakati wanamuelekeza mgonjwa akalale kwenye kitanda, wauguzi hao waliitwa kwenda kumhudumia mgonjwa mwengine mwenye Eclampisia.

Ilieleza taarifa hiyo kuwa walipokuwa wakimshughulikia mgonjwa wa Eclampisia, mama wa jamaa zake walitoka nje na baadae wauguzi walipata taarifa ya mama ameshajifungua walipoulizwa wakunga aliemsaidia mama huyu ni nani, walijibu hawamjui maana wao hawakwenda tena, ilimaliza ripoti hiyo.

Leave a Reply